Thursday 30 January 2014

Tahariri ya Tanzania Daima: Kuchapishwa kwa Rasimu ya Katiba Magazetini

Chini ya kichwa cha habari "Tume ya Katiba haikutenda haki" gazeti la Tanzania Daima limetoa tahariri ifuatayo. Inashangaza ni kwa nini Tume imeshindwa kuwezesha magazeti mengine yasiyo ya serikali na lile la Mwananchi kuchapisha rasimu ya pili. Inahojiwa pia ni kama rasimu hii imewafikia watu wenye ulemavu wa kuona?

RASIMU ya Pili ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imechapishwa jana kwenye baadhi ya magazeti baada ya kuwa imepitia vigezo vya kisheria kama alivyoahidi Rais Jakaya Kikwete wakati wa kuipokea Desemba 30, mwaka jana.

Rais aliwaahidi wananchi kuwa baada ya rasimu hiyo kuchapwa kwenye gazeti la serikali kama sheria inavyoelekeza, itasambazwa kwenye vyombo vya habari ili wapate kuisoma na kuijadili kabla ya Bunge la Maalumu la Katiba kuanza mwezi ujao.

Hata hivyo tunapenda kueleza masikitiko yetu kwamba tumeshutushwa na ubaguzi wa wazi wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa vyombo binafsi vya habari. Tunasema ni ubaguzi wa wazi na wenye nia mbaya ya kuwanyima wananchi haki yao ya kikatiba ya kuisoma rasimu na kuijadili kutokana na kusambazwa katika vyombo vichache. Rasimu hii imesambazwa kupitia magazeti matatu tu ya Habari Leo na Zanzibar Leo ambayo ni ya serikali na Mwananchi, ambalo ni la binafsi wakati yako magazeti zaidi ya 10 yanayotolewa kila siku na mengine kadhaa ya wiki ambayo kila moja lina wasomaji wake.

Kwetu huu ni ubaguzi wa makusudi wa tume ambayo kimsingi tunaamini imepewa fedha za kutosha kufanya shughuli zake ili wananchi wapate taarifa za kile kinachoendelea kuhusu mchakato mzima wa katiba yao.
Kama tume iliweza kuvitumia vyombo vyote vya habari kutoa taarifa zake na matangazo ya kuwahamasisha wananchi wapeleke maoni yao, inakuwaje leo iwanyime haki hiyo ya kupata rasimu kupitia magazeti hayo?
Hivi kwa mwananchi asiyesoma magazeti ya Habari Leo, Zanzibar Leo au Mwananchi ina maana hana haki ya kupata rasimu ili aweze kuisoma na kuijadili kwa ajili ya kuainisha kasoro kabla ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kuketi na kupitia rasimu hiyo?

Yawezekana Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji Joseph Warioba ilighafirika katika jambo hili, hivyo basi tuna imani kuwa wanaweza kulisahihisha kwa kusambaza rasimu hiyo kupitia magazeti yote ili kuwapa wananchi haki kama alivyoahidi Rais Kikwete. Tunachelea kuamini kama kigezo cha tume kutochapisha rasimu hiyo katika magazeti yote ni uhaba wa fedha, kwani tunatambua kwamba Bunge liliidhinisha mabilioni ya kutosha kwa chombo hicho ili kukiwezesha kufanya kazi zake kwa ufasaha. 

Kodi zinazotumika kutengeneza katiba zimetokana na wananchi wote, hivyo hakuna sababu yoyote ya kuwabagua katika kuwafikishia taarifa kuhusu maoni na mapendekezo yao waliyoyatoa kwa tume. Rasimu inapaswa kufikishwa kila mahala, mijini na vijijini, yako maeneo magazeti hayafiki, hivyo ni vema zikasambazwa nakala za kutosha ili wananchi waisome na kujadiliana badala ya kutaka kuwazima kwa kuwapangia vyombo vya habari vya kupata taarifa.

No comments:

Post a Comment

[ZELEZA] Malawi’s Political Earthquake: Nullification of the Presidential Elections

By Prof Paul Tiyambe Zeleza  3/2/2020 The Malawian Constitutional Court has annulled last year's presidential election results....

Most Viewed