Monday 24 February 2014

Ndani ya Bunge la Katiba: Mbowe na Marafiki wa Tanganyika

Ni siku chache tangu Bunge la Katiba lianze kazi yake mjini Dodoma. Mbali na uteuzi wa Mwenyekiti wa muda Pandu Ameir Kificho, mjadala umekuwa wa posho za wajumbe hawa. Ni aibu kubwa kwa taifa letu kuona kwamba mjadala anzilishi wa Bunge la Katiba sio wa hoja bali ya posho za wajumbe. Nimeamua makusudi kukwepa mjadala huu na hata kuchangia kwa upana. Sio jambo la kupoteza muda wako.

Nimependezwa na uledi na ustadi makini na hatua ya Mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni Mh. Freeman Mbowe kuanzisha kundi la marafiki wa Tanganyika. Waingereza wanaiita "caucus". Ni hatua madhubuti ambayo kulingana na Mh. Mbowe, itajumuisha aina mbali mbali ya makundi ndani ya Bunge hilo. Mtazamo huu chanya ni muhimu katika kuteka hoja mbali mbali ambazo zinahusu upana wa maslahi na sio ufinyu wa maslahi ya kichama, kikanda, ama hata ya kidini. Kwa mujibu wa Mbowe, kundi hili halitakuwa na chembe ya itikadi ya chama cha siasa, bali litaundwa na 'marafiki wa Tanganyika'.Licha ya mtazamo wa wazi wa Chama cha Mapinduzi kudai Mfumo wa Serikali mbili ndani ya Muungano, Mbowe anaohisi sio mtazamo wa WanaCCM wote. Misingi bora ya demokrasia katika demokrasia pevu na zilizostawi, mfumo huu wa kuleta makundi "Lobbying and Caucusing" kwa kimombo, ndio njia muafka wa kujenga maridhiano (building consensus) hata kama kuna mitazamo tofauti (diverging opinions). Ni kwa msingi huu Mbowe amependekeza uundwaji wa vikundi vya sampuli hii. 

Rai yangu kwa wajumbe wa Bunge la Katiba kujenga maridhiano kupitia makundi ya kirafiki ambayo itahusisha itikadi mbali mbali na kuleta umoja wa kitaifa. Historia inatufundisha kwamba michakato ya Katiba inaweza kuigawanya nchi kama haitaendeshwa kwa ufasaha ila inaweza kutumika kama nyenzo kuu ya kuleta watu pamoja katika maazimio ya pamoja (common aspirations) ambayo ni nguzo kuu ya katiba yoyote duniani. 
  

[ZELEZA] Malawi’s Political Earthquake: Nullification of the Presidential Elections

By Prof Paul Tiyambe Zeleza  3/2/2020 The Malawian Constitutional Court has annulled last year's presidential election results....

Most Viewed